Monday 31 October 2016

BAADHI YA MAJIBU YA MASWALI AMBAYO WATU WENGI WAMEKUWA WAKIJIULIZA

Swali: Bei ya mashine ya vigae ni kiasi gani?
Jibu: Tshs 250,000/=
 
Swali: Bei ya mashine ya matofali ya kufungamana ni kiasi gani?
Jibu: Tshs 650,000/=
 
Swali: Kama moja ya kazi ya matundu ni kupitisha mabomba ya umeme na kuimarisha kwa kumwaga rojorojo ya saruji katika kuta za kona ya jengo, kwenye madirisha na kwenye milango, Je wakati wa kumwaga zege ya lenta zege inayomiminwa si itaishia kwenye matundu?
Jibu: Nondo zinazowekwa kwenye lenta zinazuia umwagikaji wa zege inayomiminwa.
 
Swali: Kwanini isitengenezwe mashine inayotumia umeme ama Hydraulic?
Jibu: Gharama itakua kubwa sana na hivyo itaondoa unafuu wa utengenezaji tofali
 
Swali: Je kuna haja ya kupiga lipu kwenye nyumba iliyojengwa kwa kutumia matofali ya kufungamana?
Jibu: Haina lazima hasa nje. Kwa ndani ni muhimu ili kupata finishing nzuri
 
Swali: Je nyumba hizi zinadumu miaka mingapi?
Jibu: Zaidi ya miaka 45
 
Swali:Uimara wa nyumba zilizojengwa kwa kutumia teknolojia ya NHBRA ni upi.
Jibu: Sawa na uimara wa tofali za block
 
Swali: Kwanini mashine ya vigae isitumie umeme badala ya betri ya gari?
Jibu: Hii huiwezesha mashine kutumika sehemu yoyote hata isiyo na umeme (vijijini) ambako ndio kuna walengwa wakubwa.
 
Swali: Kwanini mashine ya matofali isitumie umeme ili kuwezesha kufyatua tofali nyingi kwa muda mchache?
Jibu: Inawezekana lakini Wakala unawalenga watu wa kipato cha kati na chini ili waweze kujenga nyumba bora za gharama nafuu. Mashine ya umeme itakua na gharama kubwa.
 
Swali:Kwanini vigae vinalowekwa maji?
Jibu: Kufanya viwe imara
 
Swali: Kwanini matofali yanamwagiliwa maji?
Jibu: Kufanya tofali kuwa imara
 
Swali: Kama eneo langu halina udongo mfinyanzi mwekundu, nitapata wapi udongo mwekundu?
Jibu: Sio lazima uwe udongo mwekundu, kinachohitajika ni udongo wowote mradi uwe na mfinyanzi wa kadiri ya asilimia 10 mpaka 40.
 
Swali: Kwanini matofali ya kufungamana yana matobo?
Jibu: Inapunguza uzito na inasaidia kubalansi hali ya hewa. Vile vile matobo haya yanatumika kupitisha nyaya za umeme
 
Swali: Kwanini matofali yajengwe bila udongo mwashi (mortar)? Je nyumba hiyo itakuwa imara kweli?
Jibu: Hiyo ndio aina ya tofali na teknolojia yake. Kuta za nyumba zinaimarishwa kwa nyumba kuwekwa lenta. Vilevile loki za kwenye tofali zinasaidia kuimarisha uimara wa nyumba.
 
Swali: Kwasababu gani tutumie udongo na saruji katika kufyatua matofali ya interlock na isiwe mchanga?
Jibu: Mchanga hauwezi kushikana bali udongo unashikamana ukishindiliwa kutokana na mfumo wa mashine yetu (tofali bila kibao). Vile vile mchanga hauna asili ya mfinyanzi ila udongo una asili ya mfinyanzi
 
Swali: Uzito wa vigae vya NHBRA ni kilo ngapi kwa kimoja.
Jibu: Kilo 2.6
 
Swali: Vigae vingapi vitatumika kuezeka nyumba ya vyumba vinne.
Jibu: Vigae 1700 kutegemea aina ya mchoro wa nyumba
Ni matumaini yangu tumejibu baadhi ya maswali kama kuna swali lingine au pendekezo usisite kutuandikia......

Thursday 20 October 2016

TAARIFA ZA TAFITI

Nhbra Tanzania, hutoa taarifa mbalimbali za tafiti hususani zile zinazolenga teknolojia ya ujenzi wa nyumba bora za gharama nafuu kwa kupitia tovuti http://www.nhbra.go.tz/publications/5

Tuesday 11 October 2016

MAABARA YA UPIMAJI VIFAA VYA UJENZI

Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa Vya Ujenzi Nhbra Tanzania, una Maabara ambayo inafanya majaribio mbalimbali ya upimaji ubora na uimara wa vifaaa vya ujenzi.
Kupata ufafanuzi zaidi juu ya vipimo mbalimbali vya vifaa vya ujenzi na bei zake fika Ofisini kwetu Mwenge, Dar es Salaam muda ni kunzia saa 0730-1530hrs Jumatatu - Ijumaa au tembelea tovuti yetu
http://www.nhbra.go.tz/projects/22


Fundi Sanifu akipima uwezo wa udongo kubeba mzigo "load carrying capacity" kwa kutumia mashine ya Direct Shear katika Maabara ya NHBRA


Tuesday 4 October 2016

SIKU YA MAKAZI DUNIANI

Siku ya Makazi Duniani huadhimishwa Jumatatu ya kwanza ya mwezi Oktoba kila Mwaka ambapo kwa mwaka 2016 maadhimsho hayo yalifanyika tarehe 3/10/2016 kwenye viwanja vya Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Maadhimisho hayo yenye kauli mbiu "Nyumba Kitovu cha Miji" yaliongozwa na Mhe. William Lukuvi ambaye ni Waziri wa Wizara hiyo. Katika maadhimisho hayo Wakala wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi ulipata nafasi ya kushiriki maadhimisho hayo kama mdau wa usambazaji wa teknnolojia ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu kwa kutumia tafiti mbalimbali ili kumnufaisha Mtanzania.
Arch. Godfrey Munyaga wa pili kulia akifuatilia kwa makini hotuba ya Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi kwenye maadhimisho ya Siku ya Makazi Duniani 
Mhe. William Lukuvi akiangalia bango linaloonyesha baadhi ya kazi zilizokwisha fanywa na Wakala wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi, wengine ni Afisa Masoko wa Wakala Bi. Zubeda Salum pamoja na mwakilishi wa Shirika la Nyumba (NHC) 
Mhe. William Lukuvi akipata ufafanuzi juu ya shughuli za Wakala kutoka kwa Bw. Frimin Lyakurwa ambaye ni Msaidizi Mwandamizi wa Maktaba.